Waislam, jukumu la kuanzisha Mahakama ya Kadhi ni lenu
WIKI iliyopita wakati Waziri Mkuu, Mizengo Pinda akijibu maswali ya papo kwa papo bungeni alisema kwamba serikali haijalitupa suala la kuanzishwa kwa Mahakama ya Kadhi, lakini imependekeza kuwa kutokana na suala hilo kuwa la imani, liundiwe mfumo wake ambao hautasimamiwa na dola ili chombo hicho kiendelee kuwa nguzo muhimu ya dini ya Kiislamu.
Pinda amesema kwa kuwa Mahakama ya Kadhi ni suala la imani, hivyo Waislam waiunde katika mfumo wao na serikali itatoa msaada kwa chombo hicho hadi kitakaposimama.
Amesema chombo hicho kikiundwa na kusimamiwa na dola serikali itakuwa inakiona kama chombo chake cha dola tu hivyo haitakuwa imetenda haki kwa Waislam na hata Watanzania kwa ujumla wao.
Waziri Mkuu amesema kwa kuwa inasemwa kwamba Mahakama ya Kadhi, au ofisi ya Kadhi msingi wake ni imani ya dini, hivyo anadhani si busara chombo hicho kikawekwa katika mfumo unaotakiwa kusimamiwa na dola.
Kwa kauli hiyo ya Waziri Mkuu ni wazi kwamba Waislam sasa wanapaswa kukianzisha chombo hicho wao wenyewe na kutafuta utaratibu mwafaka wa kuzifanya sheria na maamuzi yake yakubalike na jamii ya Waislam nchini Tanzania.
Binafsi nakubaliana kwa asilimia 100 na tamko hilo la Waziri Mkuu Pinda, kwani ni wazi kwamba serikali itakapoianzisha mahakama hiyo itabidi iwe ni miongoni mwa vyombo vya serikali na itakayosimamiwa na serikali yenyewe na wala si Waislam.
Serikali mwaka 1968 iliivunja Jumuiya ya Kiislam iliyoitwa East African Muslim African Society (EAMWS) jumuiya iliyoanzishwa na Agakhan na ambayo viongozi wake wengi walikuwa ni wenye asili ya Kiasia. EAMWS kama jina lilivyo ilikuwa ni jumuiya ya Waislam ya Afrika Mashariki.
Baada ya kuona kuwa Waislam wa Tanzania kwa ujumla wao hawawakilishwi vema na EAMWS na kutoa malalamiko kadhaa wa kadhaa, ndipo serikali ilipoifuta jumuiya hiyo na kuwahamasisha viongozi Waislam waliokuwa Serikalini kusimamia kuanzishwa kwa jumuiya nyengine ya Waislam wa Tanzania. Kwa msaada wa Sheikh Abeid Karume na Sheikh Rashid Kawawa waliwakutanisha masheikh wa Kiislam pale Iringa mwaka huo huo 68 na kuanzisha Baraza Kuu la Waislam Tanzania, na kwa kuwa EAMWS ilivunjwa kisheria, mali zote zilizokuwa za EAMWS zilimilikishwa BAKWATA.
Kutokana na insafu hiyo, BAKWATA kwa Waislam ikawa inaonekana kuwa ni chombo cha serikali japokuwa serikali haiwachagulii kiongozi wala haiwalipi mishahara isipokuwa hutoa msaada pale inapoombwa kufanya hivyo.
Kutokana na iktisadi hiyo na pengine matendo yasiyoridhisha au yasiyoisaidia jamii ya Kiislam kwa ujumla wake nchini, ndipo mara baada ya kufunguliwa milango ya mfumo wa kiliberali na ruhusa ya kuanzishwa kwa vyama vya kijamii katika miaka ya 1980, ndipo jumuiya nyingi za Kiislam zikaibuka kama uyoga. Nia ikiwa kuziba mapengo pale ambapo Bakwata imeshindwa na pengine kuwafanya Waislam wawe wamoja zaidi.
Baraza Kuu la Jumuiya na Taasisi za Kiislam mathalan, lililoanzishwa kwa jitihada za wasomi na masheikh mbalimbali wasiokubaliana na mawazo na matendo ya Bakwata, ilidhaniwa kuwa hilo lingeweza kujenga jumuiya yenye nguvu na kuwaunganisha Waislam wawe na sauti moja. Hadi leo Baraza hilo lina umri wa miaka 15 na bado halijapiga hatua, ndio kwanza linasimama dede na wala jitihada zake za kuunganisha jumuiya na taasisi za kiislam hazijafanikiwa kihivyo.
Jitihada nyingine za Waislam za kuwanyang’anya Bakwata mamlaka yao kwa Waislam nchini, walianzisha Baraza la Misikiti Tanzania (BAMITA). Baraza hilo hadi sasa limebakia Kisarawe tu. Waislam wanapaswa kujiuliza kwanini jitihada zao zinasuasua, watafute mbinu za kujikwamua na waache kuwanyooshea wengine vidole?
Hoja iliyopo ni kwamba ikiwa Waislam hawaipendi Bakwata kwa madai kuwa ni kibaraka wa serikali, itakuwaje kwa Mahakama ya Kadhi endapo itaundwa na kuingizwa katika mfumo wa Serikali? Je, itakuwa ni chombo cha Waislam au chombo cha Serikali?
Binafsi nadhani Waislam walikokotwa na ahadi za kisiasa zilizoanza kutolewa na Augustine Mrema wakati akiwa NCCR Mageuzi na baadaye hoja hiyo kupokwa na CCM. Ukiiangalia kwa undani wake utaona kuwa ni hoja ya kisiasa tu ambayo hujengwa kwa maslahi ya wakati fulani.
Kadhalika kuna madai ya kwamba zipo nchi zenye ofisi ya Kadhi Mkuu na Mahakama ya Kadhi ambazo zinasimamiwa na Serikali, hiyo ni kweli lakini ukiangalia utakuta kwamba idadi ya Waislam katika nchi hizo ni ndogo, hivyo serikali inachofanya ni kulinda haki za wachache (minority rights) lakini katika nchi kama Tanzania ambayo takribani idadi ya Waislam na wasio Waislam inakaribiana, kuunda chombo cha kisheria kitakachosimamiwa na dola kwa maslahi ya dini moja pengine ni hoja yenye ukakasi kidogo.
Ni kweli iko haja ya kuanzishwa kwa Mahakama ya Kadhi na ofisi ya Kadhi Mkuu nchini Tanzania lakini si haki kuishinikiza serikali kuanzisha mamlaka hizo, Waislam wenyewe wanapaswa wazianzishe na kuzisimamia, wanachopaswa kuitaka serikali kufanya ni kuzitambua tu kisheria na kutoa msaada pale inapohitajika.
Hata hivyo swali linalojitokeza ni kuwa ni nani atakayemfunga paka kengele? Swali hilo linakuja kwa sababu nchini Tanzania Waislam hawana mamlaka moja wanayoiamini na kuitegemea kusimamia mambo yao, Waislam wamegawanyika si kwa madhehebu tu bali kwa makundi na kwa taasisi mbalimbali ambazo kimsingi nyingi hazikubaliani kimtazamo.
Hawra Shamte ni mhariri wa siasa wa gazeti la Mwananchi.
hshamte@mwananchi.co.tz
0754 849694