Prof. Masha:Watanzania walijibu swali lisilo kuhusu Shirikisho
Na Hawra Shamte
MBUNGE wa Bunge la Afrika Mashariki, Makamu Mwenyekiti wa Chama cha United Democratic na Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha St. Augustine, Profesa Fortunatus Lwanyantika Masha anasema kwamba kwa bahati mbaya au kwa kutokutambua, Kamati iliyoongozwa na Profesa Samuel Wangwe haikuweza kuwaelekeza Watanzania swali halisi walilopaswa kulijibu ambalo ni je, tuharakishe Shirikisho la Afrika Mashariki? Badala yake, wananchi wakajibu swali la je, mnataka Shirikisho?
Akizungumza katika mjadala wa wazi katika Chuo Kikuu cha St. Augustine, tawi la Dar es Salaam, Prof. Masha alisema kamati ya Wangwe iliibua maoni na hisia nyingi kuhusu kazi ya kamati yenyewe; uamuzi wa kuundwa kwa Shirikisho la Afrika Mashariki; na wasiwasi wa kuunda Shirikisho la nchi zinazotofautiana kiuchumi, kijamii, kisiasa na kiusalama.
Profesa Masha anasema pengine mkanganyiko kuhusu Shirikisho unatokana na kuwapo kwa Jumuiya ya Afrika Mashariki, hivyo ili kulitambua Shrikisho la Afrika Mashariki ni muhimu kutofautisha baina ya Shirikisho na Jumuiya ya Afrika Mashariki.
“Watu wengi hawaoni tofauti baina ya jumuiya hizo mbili, na ndiyo maana kushindwa kwa EAC kunaunganishwa moja kwa moja na Shirikisho kwamba nalo laweza kushindwa kama ilivyoshindwa Jumuiya. Wasichokifahamu wengi ni kwamba malengo na utashi wa kuanzisha Shirikisho la Afrika Mashariki ni tofauti na yale yaliyokuwapo wakati wa kuanzisha Jumuiya ya Afrika Mashariki iliyovunjika mwaka 1977,” anasema Prof. Masha.
Prof. Masha anaendelea kueleza kuwa ingawa hivi sasa ipo Jumuiya ya Afrika Mashariki na ambayo kimfumo inaweza kuwa na Umoja wa Forodha, Soko Moja na Sarafu Moja bila ya kuwa na Shirikisho la kisiasa.
“Dhamira ya kuwa na Shirikisho ni kuunda Taifa Moja la watu wa Afrika Mashariki.”
Prof. Masha anasema katika utangulizi wa Mkataba wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, inaelezwa wazi kwamba: “Nchi za Tanzania, Kenya na Uganda zimedhamiria kuimarisha mahusiano yao ya uchumi, kijamii, kiutamaduni, kisiasa, kiteknolojia na mengine, kwa maendeleo ya haraka kwa nchi zote, kwa kuunda Jumuiya ya Afrika Mashariki; pamoja na umoja wa forodha na soko moja, baadaye sarafu moja na hatimaye Shirikisho la Kisiasa.”
Mkataba wa Jumuiya ya Afrika Mashariki ulishawasilishwa katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na likauridhia mwaka 2000. “Kwa maana nyingine ni kwamba; Bunge la Tanzania pamoja na Serikali ya Tanzania wameisharidhia kuundwa kwa Shirikisho la Afrika Mashariki. Kinachobakia ni mchakato wa kulifikia Shirikisho,” anaeleza Prof. Masha.
Agosti 28, 2004, wakuu wa Nchi wanachama wa EAC (Summit) waliunda kamati ya kuangalia namna ya kuharakisha mchakato wa Shirikisho ili kutimiza kwa haraka kusudio la Shirikisho la Kisiasa. Ndipo ilipoanzishwa Kamati ya Amos Wako ambayo ripoti yake ilisema kwamba kimsingi kuundwa kwa Shirikisho la Kisiasa kumekwisha anza kwani tayari miundombinu yake imeshawekwa; kuna Mahakama ya Afrika Mashariki, Bunge la Afrika Mashariki pamoja na maelewano ya mahusiano katika mambo ya majeshi, usalama na sera za nchi za nje.
Ripoti ya Wako iliweza kuainisha majukumu sita ya Shirikisho ambayo ni Ulinzi na Usalama, mambo ya Nchi za Nje, Mamlaka ya Ziwa Viktoria, Haki, Polisi na Uhamiaji, fedha na Mipango na Miundombinu.
“Ingawa wakuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki hawakuazimia moja kwa moja kukubaliana na mapendekezo ya kamati ya Wako, kwa matamshi yao walifurahishwa na kazi ya Kamati hiyo. Kwa kuwa mengi ya yaliyomo katika mikakati ya maendeleo (EAC Development Strategy 2006 – 2010) yanatokana na mapendekezo ya kamati ya Wako; kimsingi walikubaliana na programu ya kufikia Shirikisho kama ilivyopendekezwa na Kamati ya wako.”
Utata wa kazi ya kamati ya Wangwe
Kamati ya Wangwe ilihusika na mchakato wa Mashauriano ya Kitaifa (National Consultative Process) kuhusu kuharakisha Shirikisho la Kisiasa. Profesa Masha anasema nia ya kushirikisha wananchi wa Afrika Mashariki katika mchakato wa kuunda Shirikisho ni nzuri, ugumu ni namna ya kuwashirikisha na hasa baada ya maamuzi ya msingi yakiwa tayari yameisha chukuliwa. Ni taratibu zipi zitumike katika kuwashirikisha? Washirikishwe au waamue?
Prof. masha anasema pamoja na kuwa Kamati ya Wangwe ilikuwa inaratibu/inatafuta maoni ya wananchi kuhusu swali “je, Shiriksho liharakishwe au hapana?” lakini ilikuwa na utata wa aina mbili: Kwanza; mkanganyiko wa swali lililotakiwa kujibiwa. Pili; namna ya kupata maoni ambayo yanafanana na maoni ya Watanzania kwa ujumla. Yote mawili yalikuwa matatizo ya kiufundi.
Waliohudhuria mikutano ya Kamati ya Wangwe na wengi waliotoa maoni katika vyombo vya habari, walijibu swali tofauti, yaani: Je, tuingie katika Shirikisho au hapana? Kwanini?
“Tofauti hii kubwa kati ya swali lililoulizwa na swali lililojibiwa, ilileta mkanganyiko mkubwa, Waliokuwa wanaelewa vema Kazi ya kamati hiyo, waliliona zoezi lililoendeshwa na Kamati ya wangwe halikuwa na maana,”
Prof. Masha anasema.
Prof. Masha pia anabainisha tatizo jingine kubwa katika zoezi la Kamati ya Wangwe, kwamba lilikuwa namna walivyoratibu maoni ya wananchi. “Kwa mfano; walikwenda katika Wilaya yenye watu zaidi ya 300,000; wakapata ukumbi katika makao makuu ya Wilaya; wakafanya mkutano mmoja au miwili na kupata jumla ya watu 200. Maoni ya hawa 200 yana uhalali gani kuchukiliwa kwamba ni maoni ya wilaya nzima? Hawa 200 wamepatikanaje hata waweze kusemea Wilaya nzima? Anahoji Prof. Masha.
Hata hivyo, Prof. Masha anakiri kwamba jambo zuri lililotokana na mizunguko ya Kamati ya Wangwe ni kutoa mjadala katika taifa, uliosisimua kuhusu Shirikisho la Afrika Mashariki hata kama wanaanchi walijibu swali lisilo.
Mwisho Prof. Masha anatoa usahuri kuwa suala la Shirikisho ni suala la kisiasa, lenye kuhitaji maamuzi ya kisiasa. Wanasiasa hawawezi kukwepa wajibu wao wa kaumua mambo neyti kama Shirikisho, kwa kujificha nyuma ya kamati ambazo zina utata.
Mwisho.
0 Maoni ya Wasomaji:
Post a Comment
<< Rudi mwanzo